Header Ads

Rais John Magufuli amemteua Profesa Ibrahim Juma kuwa Jaji mkuu


Rais John Magufuli amemteua Profesa Ibrahim Juma kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania.

Taarifa iliyotolewa na Ikulu imesema uteuzi huo unaanza leo Jumapili.

Kabla ya uteuzi huo, Profesa Juma alikuwa akikaimu nafasi hiyo tangu Januari alipostaafu Jaji Mkuu, Mohamed Chande Othman.

Ikulu imesema Jaji Mkuu ataapishwa kesho Jumatatu saa nne asubuhi, Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais Magufuli Januari 17 alimteua Profesa Juma kuwa Kaimu Jaji Mkuu.

Kabla ya kuteuliwa katika nafasi hiyo, Profesa Juma alikuwa Jaji wa Mahakama ya Rufaa.

Jaji Mkuu mstaafu Chande hadi kufikia Januari Mosi alikuwa ameshafikisha miaka 65 ambayo ni ya kustaafu majaji wa Mahakama ya Rufani kama ilivyobainishwa katika Ibara ya 120 ya Katiba ya mwaka 1977.

Jaji Chande aliteuliwa katika nafasi hiyo na Rais mstaafu Jakaya Kikwete mwaka 2010 akichukua nafasi ya Jaji mstaafu Augustino Ramadhani.

No comments