Header Ads

Nyumba za Polisi zateketea kwa moto, familia 13 zalala nje.





Takribani familia 13 zenye jumla ya watu 44 za Polisi zimekosa makazi baada ya nyumba walizokuwa wakiishi kuteketea kwa moto jana usiku majira ya saa moja.
Nyumba hizo wanazoishi polisi zilizopo katika kata ya Sekei Jijini Arusha zimeteketea kwa moto na chanzo cha ajali hiyo kutajwa kuwa ni hitilafu ya umeme.
Mkuu wa Kikosi cha Zimamoto na Uokoaji mkoani Arusha, Andrew Komba alieleza kuwa kama taarifa zisingechelewa kulifika jeshi la zimamoto, basi huenda wangeweza kuokoa mali nyingi zaidi, “Tungefika mapema nusu ya nyumba zilizoteketea tungeziokoa,” amesema Komba.
Aidha Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo ambaye naye alifika katika eneo la tukio alilipongeza Jeshi la zimamoto kwa juhudi kubwa walizozifanya kuuzima moto huo na kuokoa maisha ya watu pamoja na mali.
“Kuna Nyumba za watumishi wetu askari zimepata ajali ya kuungua moto. Nichukue fursa hii kuwapongeza jeshi la zima moto kwa juhudi kubwa ya kuhakikisha kuwa wamezima moto huu. Takribani familia 13 zimeathirika kutokana na ajali hii ambazo zina watu kama 44….. Taarifa za awali zinaeleza kuwa ajali hii imetokana na hitilafu ya umeme..,” alisema RC Gambo.
Naye Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Charles Mkumbo amesema kuwa  tukio hilo ni janga, hivyo watakaa kuona ni kwa namna gani watawasaidia walioathiriwa.

No comments